21.7.14

TAMBUA KUSUDI LA NDOA NA NAFASI YA MWANAMKE KATIKA NDOA


TAMBUA KUSUDI LA  NDOA NA NAFASI YA MWANAMKE KATIKA NDOA
I) Ndoa kama taasisi ya Mungu.
Kwa kijana anayejitambua mara nyingi unapofikia wakati kama huu wa kutafuta mwenzi, kwake huwa ni kipindi ambacho ni kugumu sana, kwa sababu anajua anakokwenda hivyo mke kama ndiye msaidizi lazima uumize akili, lakini kwa yule asiyejitambua, huwa anaona bora kuoa yeyote yule ilimradi kampenda kwa mwonekano wake na ndiyo hizo ndoa ambazo hazidumu sana.
       Kosea nguo kuvaa, watakwelekeza ubadilishe, kosea njia watakwelekeza na utarudi, kosea kununua kiatu pengine unaweza ukabadilisha au ukauza na kununua kingine, lakini ukikosea kuoa/kuolewa, kwakweli utakuwa umeharibu dira yako na kusudi la Mungu ndani yako. Ndoa siyo kitu rahisi rahisi tu, kwa kipindi kifupi hiki ninapokuwa kwenye huduma sehemu mbalimbali hapa Tanzania huwa tunakutana na matatizo ya ndoa, hasa kwa ndoa za Kikristo ukifunga umefunga, nimejifunza vitu vingi sana mpaka nikaingia kwenye maombi nipate kujua kwanini Mungu amemua kutokutengana pindi ndoa zinaposumbua? Kwanini mara nyingi ndoa zinasumbua?

i)                    Elewa kusudi la ndoa kama kijana
a)      Ndoa yawakilisha umoja kati ya washiriki watatu wa utatu Mtakatifu (Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu). Kama vile washiriki watatu wa Utatu Mtakatifu walivyo nafsi tofauti bali Mungu mmoja, ndivyo Mume na mke ni tofauti bali wameunganishwa na kuwa mwili mmoja (Mwz 2:24).
b)      Ndoa ni mfano wa uhusiano wa Yesu na Kanisa lake (Efe 5:22-33)
a.       Mke na amtii mumewe kama kanisa linavyomtii Kristo.
b.      Mume na ampende mkewe kama Kristo alivyolipenda kanisa akajitoa kwa ajili ya kanisa.
c.       Inamana wanandoa wanapaswa kuwa mfano wa uhusiano wa Kriso na kanisa lake.

c)      Kutokana na kitabu cha Mwanzo na vitabu vingine utaona makusudi ya ndoa yalivyojitokeza.
a.      Urafiki, “BWANA Mungu akasema, si vema huyo mtu awe peke   yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye” (Mwz 2:18)
b.      Umoja, “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja” (Mwz 2:24), Kunatofauti kati ya Umoja na kuwa pamoja, umoja ina maana nia moja, lengo moja, mawazo yasiyopingana n.k. ndoa nyingi wanakuwa pamoja lakini hawana umoja, ni sawa na kwenye mkusanyiko kama msibani au harusini, kwa wale wanakuwa pamoja lakini utashangaa hawana umoja, huyu akiambiwa hivi yeye anafanya vile, mwingine anawaza ataondoka saa fulani kwenda kwake.
c.       Uzao, ‘….Mungu akawambia Zaeni mkaongezeke, mkaijaze nchi na kuitiisha;….”  (Mwz 1:28)
“Mungu akambariki Nuhu na wanawe, akawaambia, Zaeni mkaongezeke mkaijaze nchi” (Mwz 9:1).
d.      Starehe, “Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala” (Mwz 3:16),
“Uishi kwa furaha pamoja na mke umpendaye siku zote za maisha yako….” (Mhubiri 9:9)
e.       Ulinzi dhidi ya uasherati, “Lakini ikiwa hawawezi kujizuia na waoe; maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa” (1Kor 7:9)

    II) Nafasi ya Mwanamke kwenye ndoa
             Mwanamke kwenye ndoa katambulishwa kama msaidizi wa mwanamume hivyo inamaana kwamba mwanamume hawezi kujitosheleza yeye kama yeye ni mpaka kuwepo mwanamke kama msaidizi wake, na anaposema “Msaidizi wa kufanana” inamaansha “wa kukubaliana, “Mwenzi” wa mwanamume, mwenyekumkamilisha na kumsaidia, siyo kuwa mtumwa wake. Na hii inamaanisha:
i)                    Mwanaume anahitaji masaada ili kuijaza nchi na jukumu la kuitiisha nchi.
ii)                  “Msaidizi” ni cheo kikubwa na cha heshima sana.
a)      Mungu mwenyewe wakati mwingine huitwa “Msaidizi”,
“ Ee BWANA, usikie, unirehemu, BWANA, uwe msaidizi wangu”, (Zaburi 30:10),
 “……Bwana atanitunza, Ndiwe msaidizi wangu na mwokozi wangu….” (Zaburi 40:17), “
 “Hata twathubutu kusema Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini?” (Ebr 13:6),
Ukitafakari vizuri katika mistari hiyo utatambua neno msaidi limetumika kumpa nafasi Mungu anayojitokeza kwa ajili ya mwanadamu, hivyo ni kama Mwanadamu hawezi kufanya jambo bila huyu msaidizi Mungu.
b)      Roho Mtakatifu katumika kama “Msaidizi” wetu,
“Nami nimemwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele, ndiye Roho wa kweli…” (Yoh 14:16,17),
“Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia” (Yoh 14:26),
Bwana Yesu Asifiwe! Endelea kusoma na (Yoh 15:26; 16:7) .

Sasa kama hiki cheo cha “Msaidizi ni chakumstahili muumba wa ulimwengu, basi inamaana hata mwanamke anahadhi kubwa ya yeye kuwa “Msaidizi” wa mwanamume na hivyo mke inabidi ajivunie kwa kuwa nacho hicho cheo, na kama ulikuwa hujui wewe mwanaume kwa kumdharau mke wako nakushauri umpigie na magoti ukamwombe msamaha endapo ulikuwa unamdharau.
                                Itanendelea ............................................... 

NGUVU YA MTOTO WA NJE YA NDOA

 Wanyakyusa huwa tunaita (Nsighwana) yaani mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa. Huyu mtoto ana nguvu sana katika ulimwengu wa roho na mpaka kwenye ulimwengu wa kimwili, na hizo nguvu zimegawanyika kwenye maeneo mawili:
1)      Eneo la Kwanza, huyu mtoto huwa anafanyika kama lango la baraka.
Haijalishi anaishi mazingira gani, au anaishi na walezi ambao siyo mama yake wa kumzaa au baba yake wa kumzaa, pengine anaishi na bibi yake au amepanga. Lakini muda mwingine huyu mtoto, Mungu huwa anamtumia kama lango la baraka.
“Basi huyo Yefta, Mgileadi, alikuwa mtu shujaa sana, naye alikuwa ni mwana wa mwanamke kahaba; Gileadi akamzaa Yefta. Mkewe huyo Gileadi akamzalia wana; na hao wana wa mkewe hapo walipokuwa wamekuwa wakubwa wakamtoa Yefta, na kumwambia, Wewe hutarithi katika nyumba ya babaetu; kwa sababu wewe u mwana wa mwanamke mwingine. Ndipo Yefta akawakimbia hao nduguze, akakaa katika nchi ya Tobu;……….wakaenda kumtwaa huyo Yefta katika ile nchi ya Tobu; wakamwambia Yefta, Njoo wewe uwe kichwa chetu, ili tupate kupigana na wana wa Amoni”
(Waamuzi 11:1,3;5,6)
Huyu Yefta, alikuwa ni mtoto wa nje ya ndoa lakini Mungu aliachilia nguvu zake na baraka juu yake kwa ajili ya familia yake na kwa taifa zima la Israeli. Nimeona watoto, vijana wengi wanakuwa na akili sana darasani lakini ukifuatilia vizuri mmoja wapo, kuishi kwake na wazazi wake, utashangaa akikwambia anaishi na mama tu! kwani alitelekezwa na baba, na kwenda kuoa mwanamke mwingine. Wengine wanamaisha mazuri, Mungu kawabariki lakini baba alimkataa, na huko baba yake aliko maisha yake yanakuwa siyo mazuri sana. Ni wakina baba wangapi wamezaa nje ya ndoa na wamewakataa hao watoto, na maisha yao hao wazazi yakoje? Kama siyo mlevi basi atakuwa ni Malaya, ama mwizi. Mara nyingi kufanikiwa kwa hao watu ni vigumu sana, au anaweza kufanikiwa lakini nje ya njia za Mungu, kitu tunachosema ni mafanikio feki na yasiyokuwa na uzima wa milele ndani yake.
      Unamkumbuka Sulemani? Fuatilia kuzaliwa kwake ilivyokuwa. 2Samweli 12,13 (soma sura hizo). Utaona mfamle Daudi alipokuwa akitembea juua ya dari ya jumba lake la kifalme, ghafula akamwona mwanamke akioga na huyo mwanamke alikuwa anaitwa Bath-sheba, na alikuwa ni mke wa Uria aliyekuwa ni askari wa mfalme Daudi. Mfalme Daudi akafanya namna alivyofanya akampata yule mwanamke, akazini naye na yule mwanamke akapata mimba. Mtoto alipozaliwa, Mungu akamuua yule mtoto ingawa Daudi alifunga siku saba na kuomba sana. Lakini yale maombi yalikuwa yanazaa tunda ambalo Mungu alilikusudia.
v  Mungu alikuwa anamwondolea aibu mfalme Daudi kwa watu kupitia yule mtoto, endapo angeishi. Ndiyo maana mtoto alipofariki tu, Daudi akainuka na akaacha kuomba juu ya huyo mtoto.
v  Kupitia yale maombi, Mungu alikuwa anaumba mtoto mwingine atakaye mpenda, ambaye alikuja kuwa Suleimani, aliyezaliwa kupitia tumbo la huyo Bath-sheba. Ndiyo maana hata Adamu ilimgharimu sana kwa muda kuja kumzaa Sethi, ambaye atakubalika na Mungu.
Nilikuwa namuuliza Mungu, kwanini hakutokea mtoto uliyempenda kutoka kwa mfalme Daudi, aliyezaliwa mbali na tumbo la Bath-sheba? Nisikilize mzazi itakusaidia sana! Mfalme Daudi alipokuwa anazini na Bath-sheba, ujue kwamba alikuwa na wake wengine nyumbani kwake. kilichomfanya aende nje ya ndoa ni nini? Maandiko yanasema “naye huyo mwanamke alikuwa mzuri sana, wa kupendeza macho”. Inaonekana Daudi wake zake hakuwapenda kwa dhati kama huyu Bath-sheba. Mungu aliachlia mbegu iliyobora kwenye tumbo la Bath-sheba kutoka kwa Daudi kwani ulikuwepo upendo wa dhati. Unapompenda mke wako kwa dhati, ujue hata utakachokizaa kitapendwa na Mungu kwani Mungu mwenyewe ni pendo (1Yohana 4:8), hivyo unapoingia kwenye ile ibada na mkeo/mumeo msipokuwa na upendo wa dhati au mmekorofishana, au mnaingia ile basi tu! Nawaambieni mtazaa mtoto mwenye hasira, muda mwingine utashangaa anazaliwa mtoto kilema, kwa sababu mlimtafuta huyo mtoto mkiwa hamna amani wala hamkupendana kwa dhati.
    Sulemani alikuja kutumika kama mlango wa baraka ndani ya familia ya Daudi, kwani ndiye aliyekuja kukubaliwa na Mungu akae kwenye kiti cha ufalme alipotoka baba yake Daudi. Lakini kuzaliwa kwake kulikuwa ni kwa hali ambayo haikuwa halali, kwani alikuwa amezaliwa nje ya ndoa ambayo Mungu alikuwa amempatia mfalme Daudi. Fuatilia watu ambao ni viongozi mahali mbali mbali, utaona kwamba wengine walilelewa na mama tu, kwani baba alimkataa.
     Usije ukajaribu wewe mama kumtupa mtoto uliyezalishwa nje ya ndoa hata kama amekutelekeza huyo mwanamume aliyekupa ujauzito. Kumbuka Hajiri:
“Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa”
(Mwanzo 21:16,18)
Nataka uone neno hili “…Mungu akasikia sauti ya kijana..” kwa nini Mungu hakusikia sauti ya Hajiri? Mungu anapokupa mtoto kwenye wakati mgumu, haijalishi umekataliwa au la! Lakini ujue kwamba Mungu anakuwa na makusudi na huyo mtoto, la sivyo angeamua kumuua mapema, kama mtoto wa Daudi. Maisha ya baraka na mafanikio ya wazazi yanafichwa ndani ya mtoto na ndiyo maana Mungu alisikia kilio cha kijana (mtoto) ambaye alikuwa ni Ishimaili. Umewahi kufikiria, ingekuwaje endapo Hajiri angeamua kutokwenda kumchukua mwanae! Ni wasichana wangapi wametupa watoto, wametoa mimba, na wamekwama kimaisha na kiroho kwani Mungu alikuwa ameachilia baraka zao kupitia wale watoto waliowatupa.
      Wazazi huwa wanaelewa, mara nyingi inapotokea mtu kajifungua, huwa wanaelewa kuwa huyu mtoto amekuja na baraka fulani. Utashangaa wageni wanakuwa wengi nyumbani, chakula hakiishi ndani, na kadhalika. Wengine wanasema mtoto mchanga huwa anawaombea wazazi kwa Mungu kwani ni malaika, ni kweli kabisa. Mungu atamsikiliza mtoto kuliko mama au baba, na ndiyo maana Mungu alisikia kilio cha Ishamaili na siyo cha Hajiri.
       Kama ulizaa nje ya ndoa, na mtoto huyo yupo, nakushauri ukamchukue na kama hukumwambia mkeo au mumeo, ni wakati wa kumwomba Mungu akupe ujasiri na hekima ya kusema naye ili akuelewe na usivunje ndoa yako. Utashangaa umekwama kiuchumi, kumbe kuna damu inakulilia huko nje. Na uwe na uhakika huyo mtoto Mungu atakuja kumfanikisha tu, hata kama hutamchukua, na baadaye utajutia kwanini hukuwa muwazi. Unakataa mtoto, tambua unakataa baraka za Mungu.

MWENDELEZO WA SOMO

2)      Usipojua namna ya kumkabidhi Mungu, huyu mtoto anafanyika kuwa laana kwenye ndoa. 
“Gidion alikuwa na wana sabini waliozawa na mwili wake; kwa maana alikuwa na wake wengi. Na suria yake aliyekuwako Shekemu, yeye naye alimzalia mwana, naye akamwita jina lake Abimeleki.”
(Waamuzi 8:30-31)
“Kisha akaenda (Abimeleki) nyumbani kwa babaye huko Ofra, akawaua nduguze, hao wana wa Yerubaali, watu sabini akawaua juu ya jiwe moja;…”
(Waamuzi 9:5)
Abimeleki alizaliwa na Suria (Girl friend) wa Gidion, inamaana alizaliwa nje ya ndoa, lakini amekuwa mwiba kwa uzao wote wa Gidion ambao walikuwa ndani ya ndoa. Akapelekea kuwaua nduguze, watoto wa babaye Gidion.
             Nimeona ndoa nyingi sana zinavunjika kwa sababu ya watoto waliozaliwa nje ya ndoa. Zingine ni ndoa za wapendwa (waliookoka) lakini kwa kutokujua, walijikuta wakati wa ujana wao walicheza na dunia mwishowe wakazaa na watoto. Nataka ujue sababu hasa, kwanini watoto wa nje ya ndoa, wanapoingia kwenye mazingira ya ndoa halisi huwa wanasababisha migogoro ndani ya ndoa. Haijalishi amebadilika ukubwani, lakini kwanini ilete kutokuelewana kwa wanandoa na familia nzima, mara nyingine inapelekea ukoo mzima kutokuelewana na huyo muhusika (aliyezalisha).
v     Tambua yule mtoto alizaliwa chini ya agano.
“Tena mnatenda haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya BWANA kwa machozi, kwa kulia na kwa kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na kuiridhia. Lakini ninyi mwasema, ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu BWANA amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtendea mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako”
(Malaki 2:13,14)
Agano ni makubaliano, mkataba, kiapo baina ya pande mbili au watu wawili. Sasa agano ambalo linanguvu zaidi ni agano la damu, na kama ilipelekea mpaka kuzaa mtoto na huyo msichana, ina maana agano lililotendeka hapo ni agano la damu. Kama mlifanya uasherati inamana Mungu hakuwepo kwenye hilo agano, inamaana Shetani ndiye aliyehusika, maana hakuwa mke wako halali mbele za Mungu. Pindi unapomwacha uwe na uhakika lile agano linaendelea kukutafuta wewe uliyefunga na huyo msichana/mwanamume.
      Agano likitendeka la damu, mara nyingi huwa linakuwa linahitaji damu nyingine, na ndiyo mana kama imetokea ajali mahali fulani na ikaua watu, utashangaa ajali nyingine inatokea, kwani kuna mapepo yanayoendelea kufwatilia damu nyingine mahali pale. Hivyo anapotokea mtoto uliyemzaa nje ya ndoa, inamana anakuja na roho ya lile agano, likikutaka uende tena kufunga agano lingine, yaani ukaendelee kuzini, ndiyo maana inatokea hali ya kumchukia mke wako na kwenda nje ya ndoa tena, pasipo mwenyewe kujua.
v     Roho ya uasherati inakuwa inafwatilia kulipiza kisasi.
Baada ya kumwagika damu ya Habili, maandiko yanasema “….sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka kwenye ardhi” (Mwanzo 4:10b). damu ya Habili ilikuwa inalia ili kulipiza kisasi kwa Kaini. Hiyo damu inapokuja na kutaka kulipiza kisasi ndani ya nyumba, inakuwa inamuhitaji mtu aliye dhaifu kati yenu ninyi wana ndoa, ili aende kinyume na kiapo (agano) walichokifunga pale walipokuwa wanafunga ndoa. Utashangaa sana mke wa mtu anaamua kutoka nje ya ndoa na kuzini ilimradi amkomoe mume wake, kwani amemwona akiwa na wengine huko, na aliwahi kuzaa nje ya ndoa. Kitendo cha mwanamke kutoka nje ya ndoa, tayari hiyo ni roho ya kisasi inayotokana na agano alilolitenda mume wake, kwa kuzaa nje ya ndoa.
“BWANA asema hivi, Angalia nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, nami nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili”
(2Samweli 12:11)
“Basi wakamtandikia Absalomu hema juu ya nyumba darini; naye Absalomu akaingia kwa masuria ya babaye machoni pa Israeli wote”
(2Samweli 16:22)
Ni habari za mfalme Daudi, baada ya kutembea na Bath-sheba na kumpa mimba, ingawa mtoto alikufa baada ya siku saba, na alikuwa ni mke wa mtu (Uria) aliyekuwa ni askari wake Daudi. Yaani Daudi katembea na mke wa mtumishi wake, na akasababisha mimba, na Mungu akamwambia Daudi kwamba na yeye atafanyiwa kama vile vile alivyomfanyia mtumishi wake, tena pasipo siri.
v     Inafuatilia watoto.
Kumbuka Absalomu alikuwa mtoto wa Daudi, na ndiye aliyetembea na masuria wa baba yake, na si mtu mwingine! (1Samweli 16:22). Chunguza, kama baba aliwahi kuzaa nje ya ndoa, utashangaa mtoto pia anakuja kuzaa nje ya ndoa. Kama baba anazini na watoto wa marafiki zako, uwe na uhakika, watoto wake watapewa mimba na rafiki zake hao hao. Haya mambo yapo kwenye jamii tunazoishi nazo sisi wenyewe na siyo kuzimu! Ndiyo maana kila siku kizazi kinaendelea kuharibika, na kufikia mpaka miaka ya kuishi inapungua (life expand). Mtoto wa miaka kumi na mbili anazaa mtoto, yaani mtoto anazaa mtoto.
v     Inakuja na roho ya mauti.
Kuna habari nilisikia mkoa fulani, baba wa kambo alimuua mtoto kikatili sana, kwa wivu aliokuwa nao. Alimwoa mwanamke ambaye alikuwa ameshazalishwa na mtu mwingine, lakini kumbe ndani yake yule mwanamume alikuwa anamchukia yule mtoto, hatimaye ikapelekea kifo na yeye akaishia jela. Mungu atusaidie wazazi!
v     Inafunga milango ya baraka na mafanikio.
Kunakitu ndani ya familia yako lazima kitakwama tu! Mfano, utakuta familia zingine ni ngumu kupata watoto kiurahisi, kama kuna mifugo, utashangaa inaanza kudhoofika mpaka kufa, chuki kwa mke/mume wako pasipo sababu, kama unawatoto wengine, utashangaa wanabadilika akili darasani (kushuka kwa ufahamu). Mpaka unakuja kufikia wakati mtakapogundua kwamba chanzo ni huyo mtoto wa nje ya ndoa, mtaanza kusema ni mchawi na kumbe siyo mchawi bali ni roho iliyo ndani yake ambayo hata yeye anashindwa kuitambua.

Ø      Utaepukaje kama uliisha zaa nje ya ndoa? Kaa vizuri na Mungu, uvunje hiyo roho ya uasherati.
“Basi mtiini Mungu, Mpingeni Shetani naye atawakimbia”
(Yakobo 4:7)
Kumbuka kuomba toba juu yako, juu ya mwanamke uliyemzalisha, juu ya mtoto husika, pamoja na familia yako. Kuna dada mmoja, nilikuwa namfanyia maombi na shida yake kubwa ilikuwa ni ndoa haina amani, ghafla Roho Mtakatifu akaniambia juu ya mume wake kwamba ana mtoto nje ya ndoa. Naye akakiri kwamba ni kweli na amewahi kumshirikisha kwamba yupo kwa ndugu zake. Na mume wake alikuwa hatulii nyumbani, na alikuwa ana wanawake wa nje wengi sana, lakini kumbe chanzo cha magomvi yote ni yule mtoto. Tulipoingia kwenye maombi, Mungu akanipa maelekezo ya kumrudisha mtoto nyumbani ili akae na yule dada iwe familia moja.
        Unapomleta nyumbani kama familia moja, unakuwa unavunja nguvu ya ile roho ya uasherati, isiwe na nguvu, ila hakikisha umekaa vizuri na Mungu, maana utajikuta unaongeza tatizo badala ya kuondoa tatizo. Ashukuriwe Yesu Kristo yule mama akarudisha mahusiano mazuri kwa mume wake na familia nzima.
Ø      Vunja hilo agano kwa njia ya sadaka.

Kama agano lilitengenezwa kwa damu, ambayo damu ilikuwa inahusika kwenye utoaji wa sadaka. Hivyo chukua sadaka na maombi yako, nenda ukavunje hilo agano madhabahuni pa BWANA, na Mungu atasimama kwenye hilo eneo daima. Mungu alisema na huyo dada aliyekuwa anashida ya ndoa, iliyosababishwa na mtoto wa nje ya ndoa kwamba atoe sadaka. Alipotoa sadaka na nilipoanza kuiombea, ghafula nguvu za Mungu zilishuka na kumwangusha chini. Mara pepo likaanza kupiga kelele na kulalamika kwanini ametoa sadaka, kwani pepo linasema lilifunga agano na mume wake, na hilo agano ndilo lile la mtoto wa nje ya ndoa pamoja na wanawake aliokuwa akizini nao. Nakumbuka ulikuwa ugomvi mkubwa sana na ashukuriwe Yesu Kristo sadaka haikurudishwa na akafunguliwa, na ndoa yake ikaponywa.

Barikiwa sana, kwa msaada zaidi
ingia kurasa ya mawasiliano.

YATAMBUE MAMBO (7) YA KUCHUNGA SANA UNAPOKUWA KWENYE UCHUMBA/MAHUSIANO

Nilipokuwa nasoma Injili ya Mathayo sura ya kwanza, inaeleza uzao wa Bwana wetu Yesu Kristo tangu Adamu mpaka Yeye. Nikaona kwamba Yesu tunamwita Mwana wa Daudi lakini Daudi hakuwa upande wa Mariamu ambaye alimzaa Yesu, ila Yusufu aliyekuwa mchumba wa Mariamu ndiye aliyekuwa ni wa uzao wa Daudi, na ukiangalia Yusufu naweza kusema hakuusika kwa njia ya damu kwenye uzao wa Yesu bali Mariamu ambaye alikuwa ni mchumba wa Yusufu maana ndyiye aliye tungiwa mimba ya Yesu. Swali langu kulikuwa na nini mpaka Yesu akaitwa mwana wa Daudi? Yusufu na Mariamu walikuwa ni wachumba lakini hawakuwahi kushiriki tendo la ndoa mpaka Yesu anazaliwa, na alizaliwa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, sasa ataitwaje Mwana wa Daudi ambaye alikuwa ni upande wa Yusufu?
        Nisikilize! Mbele za Mungu hakuna mchumba bali kuna mke! Kipindi kile Yesu anazaliwa, walikuwepo waliokuwa bikra wengisana na siyo Mariamu peke yake, lakini kwa heshima ya Yusufu na ahadi aliyoitoa Mungu kwamba Bwana Yesu atazaliwa kwenye ukoo wa Daudi, ndiyo maana ikatokea kwa Mariamu ambaye alikuwa ni mchumba (mke) wa Yusufu. Na ndiyo maana nataka uelewe ya kuwa unapokuwa kwenye uchumba, unakuwa tayari upo kwenye mtihani wa kuingia rasmi kwenye uthibitisho wa Mungu, na ndiyo maana unapewa cheti unapofunga tu ndoa kanisani kuthibitisha kwamba umeweza mitihani ya kwenye uchumba. Na mtihani wenyewe ni namna gani unaweza ukaudhibiti mwili wako wakati wa uchumba, ni pale unapotaka kuingilia kusudi la Mungu kwa kutaka kufanya tendo la ndoa kabla ya ndoa.
        
i)                    Mtafute sana Mungu.
Mungu anapokuonesha mke/mume anamaana uendelee kumwobea na kuutafuta uso wa Bwana. Mungu anapoona moyo wako wote na upendo wako wote umehamia kwa huyo mchumba, Mungu anachofanya anawatenganisha kwa kuwafarakanisha, hicho kitu nimekiona kabisa, kuna rafiki yangu alikuwa vizuri sana kiroho alipokuwa akitafuta mke na kweli Mungu akamwonesha na akathibitisha, sasa shida iliyokuwepo ni yule ndugu alipunguza muda wa maombi, akapunguza kusoma neno, hivyo muda wote alikuwa akitumia Simu kuongea na huyo mchumba, mara baada ya miezi miwili akawa ameshuka kiroho kabisa. Mungu alichokifanya akawagombanisha kwa sababu ndogo sana iliyopelekea yule msichana kufikia kusema “sikutaki kabisa” na alidai amepata mtu mwingine, sasa ilimbidi yule kijana aanze tena kuutafuta uso wa Mungu tena, na ilimgharimu sana hadi Mungu kuanza kusema naye kama hapo awali.
         Unapoutafuta uso wa Mungu, Mungu huwa anaachilia hekima namna gani ya kuweza kuishi maisha ya ndoa, unaweza ukawa na umri mkubwa sana lakini huna hekima ya kuweza kulea ndoa na ndiyo maana utashangaa mtu anachumbiwa/anachumbia mara ghafla mambo yanaharibika, ujue Mungu hataki kuaibisha ndoa za Kikristo kwani wengi wakiingia ndani ya ndoa wanashindwa kuwa na hekima namna gani ya kulea hizo ndoa, huwa inakuwa kila siku ni kesi kwa wachungaji mara wazee wa kanisa, kitu ambacho siyo kizuri, hivyo unapopata mwenzi endelea kutafuta mapenzi ya Mungu juu ya hiyo ndoa unayoiendea.
         Tegemea kupata watoto unapoingia kwenye ndoa, kama huna mpango wa kuzaa watoto basi hilo mi sijui, lakini ninalojua moja ya madhumuni ya Mungu kufanya ndoa ni ili watu wakazae na kuongezeka (Mwanzo 1:28) au la uwe na matatizo yako binafsi. Wasichana wengi hasa wa kizazi hiki huwa wanashindwa kuwalea watoto kimaadili, pia hata uvivu wa kuwahudumia vile ipasavyo. Kuna msichana mmoja nikawa namuuliza, hivi wewe katika maisha yako ungependa kuzaa watoto wangapi na kwa muda gani? Akasema kwanza nikiolewa tu nitakaa miaka miwili bila kuwa na mtoto halafu ndipo nitaamua kuzaa, nikamuuliza kwanini? Akasema watoto ni wasumbufu sana! Huyu alionesha uvivu wa hali ya juu sana na hana ujasiri wa kuweza kukabiliana na kila jukumu lililoko mbele yake, ingia kwenye kuutafuta uso wa Bwana ili akupe hekima na ujasiri namna ya kubeba majukumu ya ndoa.

ii)                  Vunja ukaribu.
Usipende kuwa karibu sana na mchuma wako, kwa wale ambao wapo jirani au wanasali kanisa moja, na kwa wale walio mbali, siku hizi kuna Simu hivyo huwa wanaongea sana na kwa muda mrefu kitu ambacho siyo kizuri, mnapokuwa mmekuwa karibu sana kwa namna hiyo huwa Shetani anapata nafasi sana na lazima siku moja mtagombana tu! Tena kwa sababu ya Simu au meseji ama sababu ndogo tu. Kulikuwepo na rafiki yangu ambaye kila siku alikuwa anaongea na mchumba wake hata mara ishirini, kwani ilikuwa kila analofanya huwa anamwambia, sasa kijana wa kiume hakupokea simu mara mbili, yaani kilichofuata ni matusi na kumwambia umenichoka najua unawengine, sasa kwa taaarifa yako hata mimi ninao huku wengi tu! Huyo binti alikuwa akimwambia kijana, basi ikawa ndiyo mwisho wa mahusiano yao.
       Hawa wanaokuwa karibu, mara nyingi sana wanaingia na tamaa ya kufanya uzinzi, nakumbuka kijana fulani mkoa fulani sitaki kutaja, alienda kwa mchungaji na kumwambia uniongoze tena sala ya toba upya kwani nimezini, akasema alikwenda kwa mchumba wake wa kike akaingia mpaka chumbani na akajilaza kitandani, na baadaye alipokuja binti, yule kijana akaingiliwa na tamaa ya kuzini na kwa kumlazimisha yule msichana mpaka wakaweza kuzini, cha kusikitisha, wanasali pamoja na ni wapendwa ambao watu wanawaona wamesimama, na siku hiyohiyo msichana mimba iliingia. Unisikilize msichana, haijalishi unataka uimarishe uchumba au upendo kwa namna gani, maana wengine wanasema nisipomridhisha leo hawazi kunioa, wewe mwambie kama Mariamu kwamba; Yusufu ukiamua kuniacha kwa siri kwa ajili ya Yesu niliyembeba we niache, lasivyo ukubari kunioa na huyu Yesu niliye naye, usikubali kumchafua yesu ndani yako.
       Usikubari mzoeane sana, kwani mtakapoingia kwenye ndoa mtajikuta ni watu kama wa kawaida tu (dada na kaka), kiasi kwamba unatakiwa unapoingia kwenye ndoa kila mmoja anamwona mwenzake kuwa mpya, mkizoeanana sana inafikia baadaye mnakinaiana na mpaka inafikia kudharauliana hatimaye kila mmoja ataanza kuona mwenzake kama siyo chaguo lake mwishowe kuvunjika kwa uchumba.
       Mnaweza mkawa mnafanya kazi ofisi moja, itawabidi mtengeneze nidhamu ya kipekee sana. Nakumbuka tulikuwa nchi fulani sitaki kuitaja, tulikuwa kikazi na tulikuwa watu wengi kidogo kwani tulienda kwa ajili ya semina, sasa katikati yetu kuna watu walikuwa ni wachumba, cha ajabu ni pale wakati wa kwenda kulala, na kwa sababu tulifikia Hotelini ilikuwa ni lazima tulale tofauti tofauti, sasa wao ilikuwa ni kitu kigumu sana ndipo wakataka kutumia nafasi ile kufanya ufuska wao, ikapelekea kila mmoja wetu akagundua ule mchezo waliokuwa wanataka kufanya, mpaka wakakalishwa kikao na wasimamizi. Sasa ni aibu sana kwa picha kama hii na inaonekana nidhamu hawana.

                                                  MWENDELEZO WA SOMO
              Ukisoma Mathayo 1:18-25, Utapata habari za Yusufu na Mariamu mama yake na Yesu, utagundua kwamba baada ya Yusufu kumwona Mariam anaujazito wa Yesu na hawajawahi kukutana kimwili, lile jambo lilimfanya Yusufu aanze kumwacha kwa siri Mariamu. lakini kile kitendo cha Yusufu kutaka kumwacha Mariam kilimpa Mungu nafasi ya kumthibitishia Yusufu uchumba wao, na Mungu alisema usimwache mkeo! na Yusufu akajirudi, lakini fikiria Yusufu angeamua kukaa tu naye kwa sababu ya kupenda lakini akiwa na kinyongo ndani yake kwamba Mariam amepata mimba nje ya ndoa ingekuwaje! Mungu aliamua kusema kwa sababu Yusufu alijaribu kujitenga na Mariamu. hivyo unapovunja ukaribu na mchumba wako inampa nafasi Mungu kusema na kufanya jambo katika mahusiano yenu, na kama siyo wa kwako itajulikana hapo. wengi wameoana na siyo makusudi ya Mungu bali ni kwasababu walijiambatanisha wao kwanza na Mungu akawa hana nafasi ya kusema nao.


iii)                    Ukweli na uwazi
Wakati wa uchumba ndiyo kipindi ambacho utatakiwa kumchunguza na kumfahamu mwenzi wako, wapi ni mdhaifu na wapi yupo imara, kusudi ujipange namna gani ya kumsaidia pindi utakapoingia kwenye ndoa, na endapo mwenzako hatakubaliana na udhaifu utakaokuwa nao, basi huyo Mungu hakukusudia mje kuishi pamoja. Kijana mmoja tulikuwa wote chuoni, alikuwa na mchumba wake na wote wameokoka vizuri sana, sasa ghafla akaja akaniambia “nataka nikwambie kwamba fulani siyo mchumba wangu tena!” Mi nikashangaa, kwani hawa watu tayari hata nyumbani kwao wanatambuana, aliponipa sababu akasema mimi sikujua kwamba mtu mzima kama yule anaweza akawa anakojoa kitandani, na juzi ndiyo nimejua napo hajaniambia yeye! Nikashangaa sana kiasi kwamba nikaona kwamba Mungu hakupanga hawa wawili waje kuishi pamoja, kwani hiyo ni sababu ndogo sana, na inamana angekuwa ni yeye je!
       Kuna mambo mengine ambayo ni muhimu wakati wa uchumba kuweza kuambiana ukweli na mengine siyo uyafunue, haswa ya kifamilia. Ndoa nyingi zimekuja kusumbua kwa sababu baada ya kuingia kwenye ndoa ndipo unakuja kutambua kwamba kumbe mmojawapo anamtoto tayari huko nje, na hakukwambia mpaka mmekuja kufunga ndoa. Huwa yanatokea sana siku hizi, na kwa sababu vijana wengi wanaonana mjini au chuoni, ghafla wanapendana na wanafikia mpaka ndoa hata bila kujua historia ya mwenzake huko walikotoka. Fikiria ndiyo mnaenda kusalimia na kutambulishana kwa wazazi kijijini baada ya kuoana, sasa ndiyo unakutana na familia ya huyo mwanamke/mwanaume si utazimia!

iv)                  Usitumie udhaifu wa mwenzio
Uchumba siyo kuumizana, msiingie kwenye ndoa mkiwa na vidonda vilivyotokana na kipindi cha uchumba. Hizi hali huwa zinatokea sana, kijana wa kiume anapoufunua upendo wake kwa msichana, na pindi msichana anapotambua kwamba anapendwa sana na mchumba wake, huwa kinachotokea yule msichana anadiriki kumwendesha mwenzake kwa kila hali, analosema anataka ndivyo iwe hivyo. Muda mwingine anajaribu mpaka kumwmbia ya kwamba mi ntakuacha endapo wakizozana kidogo, sasa vitu kama hivyo baadaye vinaleta athari kwenye ndoa. Kuna ndoa niliwahi kuiona mkoa fulani yaani mwanamume anapigwa na mke wake, kisa yule mwanamke alikuwa ni mzuri sana wa sura, sasa mume wake alikuwa amempenda sana mke wake hivyo anaona bora apigwe tu lakini mke aimwache. Ndoa nyingine niliona mwanamke alikuwa na hela kuliko mwanamume, sasa inapofikia wakati wa kupika chakula alikuwa anaambiwa mwanamume akapike.
      Mshukuru Mungu pale mwenzio anaonesha upendo wa dhati kwako, nawe jitahidi uoneshe upendo kwake, kunawengine wanatamani sana kusikia hata neno “I love you”  kwao ni adimu sana. Sasa wewe unaambiwa kila dakika hayo maneno na yanakupa kiburi cha kumnyanyasa mwenzako, muda mwingine unaweza ukawa unajaribu kama kumpima, lakini kumbe nawe unampenda kweli, sasa siku akaamua kukata tama na mawasiliano ndipo utakapotambua thamani yake.
“Mwanamke akamwambia, wawezaje kusema nakupenda; na moyo wako haupo pamoja nami? Umenidhihaki mara hizi tatu, wala hukuniambia asili ya nguvu zako nyingi” (Waamuzi 16:15)
Ni habari za Samsoni na Delila, na maneno hayo alikuwa akiyasema Delila akimwambia Samsoni pale alipokuwa anahitaji kujua asili ya nguvu zake, hivyo Delila alijua hana namna yoyote ile ya kumbana Samsoni ili aseme asili ya nguvu zake, lasivyo amwambie suala la upendo kwamba akiendelea kumdanganya basi Delila ataachana na Samsoni, na kwa sababu Samsoni alimpenda sana Delila hivyo ilimlazimu Samsoni kumwambia siri ya nguvu zake. Ndivyo ilivyo siku hizi, kijana akimpenda sana msichana huwa anabanwa sana mpaka hela zote zinakwenda kwa msichana hata kabla ya ndoa.

         Wasichana wengine huwa wanapokuwa na marafiki zao, huwa wanatabia ya kulingishiana wachumba zao, kwamba yupi anapendwa sana na mchumba wake. Wanafikia mpaka kushindana kwamba “mimi wa kwangu ana hela, nikimwomba hata saizi alfu hamsini anatuma” na wanaamua kuomba kwa huyo mchumba wake, na asipotumiwa atakuwa ameaibisha na anajikuta anaingi kumchukia mchumba wake kwa sababu ya kijinga. Na uelewe unapojitangazia kwa wenzako kwamba unapendwa sana, sasa kwa taarifa yako kunawasichana wanamapepo ya kupenda wanaume wa wenzao, utashangaa kesho mchumba wako yupo na rafiki yako.

INAENDELEA





 +255 (0) 712 201 073/ +255 (0) 752 005 418

YAJUE MAMBO SABA (7) MUHIMU YA KUTAFAKARI NA KUZINGATIA WAKATI UNAFIKIRIA KUOA/KUOLEWA

Maisha ya ndoa ni maisha ya kipindi cha mwisho kwa Mwanadamu kilicho na mitihani mingi sana, kwani ni darasa tosha kwa wanandoa, na ndiyo maana katika uchumba unatakiwa upitie misukusuko kwani ni mojawapo ya mitihani ili ufikie kupata cheti wakati wa ndoa, na nikatafakari sana kwamba hapa duniani mwanadamu anapata cheti baada ya kufaulu mitihani, lakini kwa ndoa nikashangaa mtu anapewa cheti kwanza ndipo anapoingia kwenye mtihani wa maisha ya ndoa, sasa ni wewe kufaulu au kushindwa! Hivyo ili kuweza kuishi maisha ya ndoa yaliyo mazuri na yenye furaha ni vyema katika uchumba ukajua namna ya kujibu maswali kwenye mtihani ulio nao (Uchumba kama mtihani, na cheti ndicho kinachowakilisha kufaulu kwako na ndipo unaingia kwenye maisha ya ndoa, Haleluya!!) 

  1. Tambua unapoamua kuoa au kuolewa unakuwa unaunganisha familia tatu tofauti na zenye maagano tofauti.
Familia ya kwanza ni yenu nyie wawili yaani mke na mume, siyo rahisi kuweza kuishi kiraisi na mtu ambaye amelelewa kwao na mazingira tofauti na ya kwako, malezi tafauti kabisa, mawazo na mtazamo ni tafauti, mara ghafla mnaanza kuishi pamoja, na mnatakiwa kuwekana wazi kwa kila jambo na kufanya maamuzi yasiyoweza kuwafanya mgombane. Sasa katika nyie wawili mtegemee kujenga na kuzaa familia yenye mtazamo na taswira tofauti na familia zenu mlikotoka. Na familia zinazokuja hizi mbili ni upande wa mwanamke na upande wa mwanamume na kila familia ina tabia zake.
         Familia zingine badala ya baba kuwa kiongozi wa nyumba, utakuta mama ndiye kiongozi wa nyumba, inamaana kila analosema mama pale nyumbani ndilo linafwatwa, wala baba hawezi kuwa na maamuzi yoyote yale juu ya uamuzi atakaoufanya mama, sasa chukulia ndiyo unaoa msichana kwenye hiyo familia na ghafla anaanza kukuendesha na kuwa na sauti ndani ya nyumba kwa kila kitu, na kwa sababu alikotoka kwenye familia yao ameona mama ndiye kiongozi na mwenye sauti ya mwisho wa familia, na kwa sababu wewe mwanamume hayo mambo kwako ni mageni basi lazima muingie kwenye ugomvi.
         Umewahi kufikiri unaenda kuo/kuolewa kwenye familia ambayo ni wachawi! Vijana wengi kwa sababu ya tamaa zao wamejikuta wameishia kuoa/kuolewa na watu wachawi. Kuna kijana mmoja alikuwa ni mtumishi mzuri sana na Mungu alikuwa anamtumia vizuri sana lakini ilipofika kipindi cha kuoa akaaamua kuchagua binti fulani kanisani humohumo na huyo binti alikuwa anaonekana yupo safi kiroho na alikuwa mzuri hata wa sura, lakini watu walimshauri kwamba huyo binti hakufai na kwa huduma uliyonayo kwa kweli itakufa. Yule mtumishi hakuweza kuelewa ushauri wa wale watu, alin’gan’gana mpaka akamwoa yule binti na ilipofika kipindi wanapokuwa kwenye huduma vijijini pamoja na watumishi wengine, yule mtumishi akawa anashindwa kutumika kama hapo awali, mara Mungu akamfunulia mtumishi mwenzake, usiku akamwona yule mtumishi anakabwa na mke wake mpaka anaelekea kufa, ndipo wakatambua kwamba yule binti alikuwa siyo mzuri yaani alikuwa mchawi, basi mpaka sasa yule mtumishi anaishia kuwa kama waumini wengine kanisani kwani huduma ndiyo imekwisha kabisa mpaka sasa.
        Familia zingine huwa ni wachafu sana, yaani siku ukaenda nyumbani kwao ghafla bila taarifa, utashanga takataka mpaka mlangoni na mara nyingine hata kupiga deki ndani ni shida tupu, sasa unajiuliza humu ndani naingia nivue viatu au? Maana nikivua ni lazima nitachafuka na nisipovua watasema hana adabu. Sasa umewahi kufikiria ndiyo mwanamke anakuja unamwoa utashaagaa hata kitanda kutandika ni shida, nguo zinakaa mpaka sebuleni. na wanaume, siku mke kasafiri utajua tu kwamba leo mke wa fulani kasafiri, utashangaa kuona sebuleni pako ovyo, vitambaa ni balaa tupu utasema kunawatoto walikuwa wanacheza na kama alikuwa anajipikia basi utavikuta vyombo vimejazana na vinazungukwa na nzi, sufuria zina masizi mpaka ndani sasa sijui yaliingiaje mi sijui! Ni aibu hiyo jamani!, sasa hali ikiwa kama hivyo itapelekea magonjwa yasiyoeleweka. Badala ya kuona raha ya ndoa sasa unaanza kuona karaha ya ndoa kisa hukufanya uchunguzi na kufikiria kabla hujafanya maamuzi.
       Watu wengine ni wavivu sana, maandiko yasema “asiyefanya kazi na asile”, kunafamilia zingine jamani ni tabu tupu, ukiangalia wanapenda kuvaa vizuri sana na kujipenda sana na kanisani wanaenda sana, lakini ukiuliza wapi wanashamba la kulima watakwambia hamna. Kweli wengine wanaishi mjini mashamba ambapo hamna lakini nina maana hata sehemu ya kujipatia riziki angalau kidogo, wengine hata kujishughulisha na shughuli ndogondogo tu huwa hawawezi, hasa vijana wa kiume utashanga kuanzia asubuhi mpka jioni anaangalia Vidio (Television Vidio (TV)) na hapo anamchumba na anapanga kuoa, hata godoro hana na bado anakaa kwa wazazi wake, yeye huwa anasubiri asubuhi ifike anywe chai aliyopika mama au dada ndipo aende kijiweni na ikifika mchana atarudi kula chakula cha mchana na kurudi tena kijiweni, hivyohivyo na jioni na kama ndiyo siku ya ibada ndipo ataoga na kuomba sadaka kwa mzazi halafu aende kanisani. Mhh Mungu atusaidie sana.
       Familia zingine zinamazindiko sana, kwamba kila atakaye mwoa huyu binti wa kwanza ni lazima afe, au wanamwapisha kwamba huyu binti atakuwa anaishia kuwa mjane, pia hata upande wa mwanamume huwa mazindiko yapo, kwamba huyu kijana kila akioa hatakuwa anapata watoto. Nilipigiwa simu siku moja na binti, akaniambia nimwombee kwani alinenewa na shangazi yake ya kwamba hatakuja kupata mume wala mafanikio yoyote katika maisha yake yote, na hapo alipo alikuwa amewahi chumbiwa mara tatu na anaishia kuachwa pasipo na sababu, na sasa anaishia tu kukaka kwa dada yake, usije kushangaa hata mwenyewe unajaribu kupanga kuoa/kuolewa kumbe umefungwa lakini yote ni ushirikina wa kifamilia au huo ukoo.
       Pia kuna familia zingine au makabila mengine huwa wanadai mtoto wa kwanza kuzaliwa ili atolewe kama kafara, na usipoelewa hili litakugharimu pindi tu utakapokuja kumpoteza huyo mtoto na ndipo utakapoelewa, na ndiyo maana tunasema kijana kaa vizuri na Mungu naye atakupa macho ya rohoni utaona wapi panafaa kuoa/kuolewa. Kumbuka pia magonjwa mengine ya kurithi huwa yanafwatilia watoto wa kwanza kama vile kuugua kichaa, kifafa, kifua kikuu, UKIMWI n.k na hizo zinakuwa ni roho tu zinazofuatilia familia. Kumbuka unapounganisha mambo yote ya familia ya upande huu na upande mwingine unategemea utapata nini hapo?

  1. Unapoamua kuoa/kuolewa utambue unaenda kuwajibika zaidi
Kumbuka ya kwamba unapoamua kuoa/kuolewa unaenda kuanza maisha ya kipekee kwani hiyo ndiyo ngazi ya maisha yako ya mwisho mpaka kufa kwako, kumbuka siku utaitwa baba/mama mpaka utakuja itwa bibi/babu, kama Mungu atakujalia maisha marefu, hivyo kumbuka utakuwa umekusanya ndugu wa pande mbili zote, sasa usije sema mi naweza nikamlea mke wangu tu! Hapana, kumbuka kuna ndugu wa upande wa mke/mume wako watahitaji msaada je utaweza kumudu? Na maandiko yanasema;
“Lakini mtu yeyote asiyewatunza walio wake, yaani wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini” (1Timotheo 5:8)
Ni aibu na ni dhambi, pale unaposhindwa kuwahudumia ndugu zako wa nyumbani mwako, kumbuka kunamaradhi, kuna misiba, kuna wengine wanasoma kama mdogo mtu au kaka mtu hao watahitaji matumizi ya shule au ada, kuna mambo ambayo ulipokuwa peke yako uliona ni rahisi kufanya lakini pindi unapokuwa na ndoa unatakiwa kuwajibika zaidi.
       Mara nyingine kwa kijana wa kiume unaoa msichana ambaye ni wa kwanza kwao au ni tegemeo kwenye familia yao, na pindi unapoamua kumwoa inamaana tegemeo lote linakuwa ni wewe, sasa sikwambii usimwoe! Hapana, baali hakikisha umejipanga vizuri kukabiliana na majukumu aliyokuwa nayo kwao kwani huwezi kuwatupa ndugu wa upande wake, na siku nyingine watapenda kuja kukutembelea kwako, na wengine watapenda kulala kama ni mbali kidogo, sasa itategemea umejenga nyumba au umepanga nyumba ya namna gani, nasema hivi kwani nimeona pindi tu wanandoa wanapoingia wakiwa hawana hata muda mrefu huwa inaanza misuguano na ukifwatilia utakuta ni ndugu wanajaa nyumbani. Sasa jiandae unaeingia kwenye ndoa kubeba ugeni na kuwajibika kwa hali na maali.
        Kumbuka kunakuwajibika kimawazo pia, muda mwingine kunakuwepo na vikao mbalimbali vya familia ya upande wa mwenzi wako, nawe kama mwanafamilia unatakiwa kuwa na upeo wa kuweza kuchangia hoja na mawazo ya kimsingi, utashangaa shemeji mtu kwenye kikao anakuja ananuka pombe na anayoyafanya pale kwenye kikao mwenyewe mwenzi wake utatamani uzimie. Sasa kama yeye mwenyewe anashindwa kujilekebisha ataweza kweli kumpa mtu mawazo ya kumjenga? Na ndiyo hao wanafika kipindi wanatembea na wafanya kazi wao wa ndani na inayopelekea mpaka ndoa kuyumba.
        Hasa kwa mabinti nataka mnisikilize, ni aibu sana binti unaeingia kwenye ndoa halafu hujui kupika, unapika wali jinsi unavyoukologa loh! Utazani unakologa uji, na ukipika ugali unaekula utatakiwa uwe na maji ya moto pembeni kwani lazima ukutane na mabonge ya unga katikati ya ugali, sasa ni aibu na ndiyo maana wanaume wanaamua kula huko nje ndipo wanarudi nyumbani. Pia wanaume nanyi mnashangaza sana wengine hata kusonga ugali ni shida sana, na pindi mke anumwa wewe unaamua kununua chipsi, sasa sijui mtakulahizo chipsi mpaka lini, siku umeingia jikoni unaipua ugali mbichi kabisa. Nakumbuka nilitembelewa na rafiki yangu mmoja na mimi nilikuwa sishindi nyumbani, na pale nyumbani kuna kila kitu cha kuweza kupika, siku nimetoka kazini narudi nyumbani nikakuta hajapika kitu, nilipomuuliza mbona hujapika? Na umekula nini? Akasema nilinunua chipsi, nami nikajua aliamu tu kununua chipsi pengine kwa sababu ya uchovu, sasa kesho yake nikamwabia twende sokoni ukaje na mboga kwani mimi sitarudi! Tulipofika sokoni nikanunu mboga na nilipomwambia aendelee kupika, akasema utakuja kupika mwenyewe kwani mimi sijui kupika! hah! Yaani nilishikwa na butwaa, na nikweli kabisa alikuwa hajui na alikuwa kijana amemaliza chuo kikuu.
       Sasa unielewe kwamba unapooa unaenda kuwa na mipaka, kwamba ni lazima ukawajibike tu na hiyo mipaka ni ya baadhi ya mambo mengine kutokuyafanya, kama vile kurudi usiku nyumbani, kama ulikuwa unakesha kuangalia mpira kwa jirani yako sasa itabidi hiyo tabia ife, kwani siku utarudi utakuta mwana si wako.
        Kama bado hujaoa, weka mpangilio ni lini unaoa kusudi upangilie mipango na namna gani utaweza kukabiriana na majukumu, shida ipo sana kwa vijana wakiona fulani kaoa basi utashangaa naye huyu anakimbilia kuoa, we unajua mwenzio alivyojipanga? Weka malengo ndani ya muda fulani utakuwa umefanya mambo kadhaa ndipo uingine kwenye ndoa.
“Kwa kila jambo kuna majira yake na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu”
 (Mhubiri 3:1)
Ujue kila kipindi unachopitia kuna takiwa uchukue hatua za mabadiliko kutegemeana na majira, na kama unajipanga kuoa baada ya miaka miwili inamaana kunamambo utatakiwa kuyafanya hapa katikati ili kujiandaa kukabiriana na majukumu ya ndoa. Pia kwa kadri tathmini utakavyokuwa unaiona ni rahisi kuwa na taswira nzima ya ndoa yako na kujua watoto utakao kuja kuzaa. Kunawengine wanaingia kwenye ndoa hata hawaelewi watazaa watoto wangapi na wengine hata wakati wa uchumba huwa hawajadili kwamba waje wazae watoto wangapi, sasa inapotokea mmeingia tayari kwenye ndoa na mwenzio anataka watoto sita na wewe unataka wawili sasa sijui mtakata rufaa wapi, mimi sijui! Zaidi mtakuwa mnaleta kuvutana kwenye suala la idadi ya watoto kila siku.
        Unapoamu kuoa angalia kwanza wewe ni tegemeo kwenye familia au lah! Unawadogo zako wanatakiwa kwenda shule na bado hawajaenda au ndiyo wapo shule, elewa unapoingia kuoa kabla ya hao watoto kuwawekea msingi mzuri ukitegemea kwamba ukioa utawasomesha, uwe na uhakika kabisa watayumba kwani maamuzi yako ya kuwasomesha ukiwa kwenye ndoa ni lazima umshirikishe mke wako, na siyo rahisi kukubali kila mwisho wa mwezi mshahara uende nyumbani kusaidia ada ya wadogo zako, na mara nyingi familia zimekwama kielimu na maendeleo mengine kwa sababu tu kaka aliyekuwa mwenye uwezo kaoa na baada ya kuoa akasahau kusaidia wazazi na wadogo zake.


INAENDELEA

iii. Unapoamua kuoa/kuolewa kuna baadhi ya marafiki utajikuta mnatengana au mnaungana.
Ukisoma (Hesabu 12:1-2)
“Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi, wakasema, Je! Ni kweli BWANA amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao
Ukiendelea kusoma mistari huko mbele, utaona Mungu anaingilia kati na hatimaye Miriamu anapigwa na Mungu kwa pigo la ukoma kwa sababu waliingilia ndoa ya Musa kwa kumsema vibaya mtumishi wa Mungu. Ni muhimu sana kabla ya kuanza kuwashirikisha watu juu ya mchumba amabye pengine Mungu kakuonesha, sasa unahitaji uthibitishe angalau kwa watumishi wenzako nao waombe waone kama ni mpango wa Mungu au la!, sasa umewahi kufikiri Musa angewashirikisha hao ndugu zake kabla hajaoa! ni lazima wangempinga tu!
       Ni muhimu sana uelewe mapema kwa kuchunguza marafiki wa mtu utakaeoana naye, kusudi baadaye isije ikaleta shida kwenye ndoa, kuna baadhi ya marafiki hawawezi kukushauri uoane na fulani pengine ya chuki zao binafsi, sasa itakapofikia baadaye mmeoana tayari tambua hawataweza kuendelea kujenga tena urafiki na ninyi, hivyo itapelekea chuki isiyokuwa na maana. Kikubwa ni kuchunga sana marafiki wanaokushauri juu ya mtu wa kuoa, je! kunauhusiano gani na huyo unaetaka kuoana naye?
      Wajue mapema marafiki wa mchumba wako mapema, na kama ni wazuri itabidi uendelee kumshauri awe nao lakini kama umechunguza ukaona wanakasoro itabidi uingine kwenye maombi Mungu akuongoze namna gani umshauri ili aweze kuachana nao. nimeona kuna marafiki ambao wanakuwa ni kero baada ya mtu kuoa na wengine wanadiriki kuwataka kimapenzi wake za rafiki zao, hiki kitu ni cha kukiangalia vizuri na hasa kwa marafiki wengine ambao ni walevi na wavuta sigara, inapofikia mchumba wako amebadilika kama alikuwa na hizo tabia kabla ya uchumba na akawa bado anao hao marafiki uwe na uhakika pindi mtakapooana atashawishika kurudi kwenye zile tabia za zamani kama marafiki zake.
      Na mara nyingi sana nimeona watu wakiwa wanawashirikisha marafiki zao sehemu ya kuo/kuolewa huwa haohao marafiki zao wanawageuka na kuanza kufanya mahusiano wao. Ukiona sehemu kunakiota cha ndege usije ukaenda kuomba msaada namna gani ya kumla kabla hujamkamata utaishia kusema ilitakiwa iwe mimi!
      Kumbuka namna ya kujinasua kwenye huo mtego, utashanga hadi unahama mji, na ndiyo maana watu wakioa tu, wanaamua kuhama miji ya kuishi, na ni muhimu sana ili kuondoa mazingira yale ya zamani ambayo yangeweza kukuwekea vikwazo kwa baadhi ya watu jinsi walivyokuzoea, kwa mfano kama ulipanga nyumba, utambue kuna majirani wataendelea kuja na pengine walizoea kuangalia Vidio (TV) ndani kwako mpaka usiku, kitu kitakachopelekea kumkwaza hata mke wako. Sasa inapotokea umeoa ni bora uhame na itabidi mkubaliane sehemu ya kuishi baada tu ya ndoa kusudi msije mkapishana kwa ajili ya mazingira ya kuishi, wengine wanaamua kwenda mkoa kwa mkoa sasa kama mke anataka Mwanza na mume anataka Mbeya, si ndiyo chanzo cha kuvunjika kwa ndoa, kumbe ni bora mkubaliane mapema kabla ya ndoa ili mmoja wenu akigoma kuhama kutokana na sababu zake binafsi muwe tayari kutokuoana. Lakini wengine hawataki kuhama kutoka Buguruni kwenda Ubungo ila yeye anataka Gongolamboto sasa ni bora makubaliano mapema, kwani muda mwingine anakataa kuhamia huko kumbe wakati bado hamjaoana aliwahi kuolewa huko na akaachika, pengine amewahi kufumaniwa mazingira hayo, si unajua ndoa za siku hizi vijana wanaonana kwenye daladala tayari wanapendana na kesho wanatangaza harusi bila hata kumchunguza vizuri mwenzake.

iv. kuoa au kuolewa kunaweza kukakubadilisha  utumishi wako.
“Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakaugeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa BWANA, Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake”
(1Wafalme 11:4)
         Ukisoma mstari wa 3 utaona idadi ya wake aliokuwa nao Sulemani, alikuwa na wake mia saba na masuria mia tatu yaani wake wa nje ambao wanajulikana kwamba anatembea nao, na wote hao wake walikuja siyo kwa sababu ya uzuri wa sura yake, maana maandiko hayajasema lakini kutokana na maandiko inaonesha ni kwa sababu ya utumishi aliokuwa nao pamoja na hekima aliyokuwa nayo, hivyo unapokuwa mtumishi angalia hata watu wanaotaka ushauri kutoka kwako wasije wakawa wanataka kuteka utumishi wako. Sulemani na hekima yote ile ambayo aliambiwa na Mungu kwamba hayupo na hatakuja kutokea Mfalme kama wewe na hatima yake anaishia vibaya na utumishi wake.
“Samsoni akaenda Gaza, akaona huko Mwanamke kahaba, akaingia kwake……….Wafilisti wakamkamata wakamn’goa macho; wakatelemka naye mpaka Gaza, wakamfunga kwa vifungo vya shaba; naye alikuwa akisaga ngano katika gereza”
(Waamuzi 16:1;21)
Najua unamkumbuka Samsoni ambaye alikuwa amemwoa Delila, Delila aliingia kwenye ile ndoa akiwa na jambo moja tu! Na lilikuwa ni namna gani ya kuharibu kusudi la Mungu ndani ya Samsoni, Shetani anawinda sana kusudi la Mungu ndani ya mtu hasa anaye jua kabisa kwamba atakuwa ni Lango la Familia, Nchi, n.k na atahakikisha anatumia mke utakayemwoa kusudi akubane, wapo watumishi wamekwama kihuduma kwa sababu ya vikwazo vywa wake zao. Kuna dada fulani alikuwa safi sana kiroho lakini akaja akaolewa, ghafla kanisani akaachishwa kwenda na mume wake.
        Mara nyingi Mungu huwa anaachilia kusudi (hasa huduma) kwa mwanamume, pia kwa mwanamume huwa linajidhihirisha kwa urahisi na huwa ni wepesi kutambua wito wao lakini mwanamke zile hisia za kudhihirisha huwa zinakuwa mbali, na ndiyo maana utashangaa utumishi unachanua baada ya kuolewa tu! na tena kaolewa na mtumishi ndipo utatambua. Sasa Shetani anachofanya kwa mwanamume huwa anakusogezea Delila au Mke wa Ayubu kusudi aharibu kile Mungu anachotaka kichanue.
       Inavyoonesha Delila alikuwa ni mzuri sana wa umbile la nje na sura, na ndiyo maana alikuwa kahaba (anajiuza), na siku hizi vijana wanaangalia sura na umbile la mwanamke na ajabu yake wanabeba akina Delila hatimaye ndoa zinaishia robo ya safari, nataka nikwambie mke siyo sura nzuri wala umbile zuri, baali ni moyo wake. Nakumbuka kuna rafiki yangu tulipita mahali fulani halafu ghafla tukakutana na rafiki yake huyo rafiki yangu, na yule rafiki yake alikuwa na mke lakini kwa mwonekano wake alikuwa hawaendani, ninamaana mwanamume alikuwa kidogo anamwonekano mzuri (Handsome) kuliko mke wake. Sasa yule rafiki yangu akaniambia “huyu jamaa utazani alichagua mke akiwa amesinzia?” “nikamwambia jipange tena kuongea maneno hayo” na yeye alikuwa bado hajaoa, nikamwambia usitukane mamba kabla hujavuka mto, siku ukijakumwomba Mungu akupe mke akakuletea asiyekuwa na pua sijui utasemaje! Na huwezi kukata rufaa ya maombi.
“Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; Bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa” (Mithali 31:30)
      Mwanamke anaweza akawa mzuri sana lakini akawa kikwazo kikubwa kwenye ndoa yako, utumishi wako/katika mahusiano yako na Mungu, pia huyohuyo mwanamke anaweza akawa ni nguzo nzuri kwenye huduma yako inategemeana umesugua goti kwa namna gani kumwomba Mungu akupe atakaekufaa.


v. Kuoa/kuolewa kunakutenganisha na wazazi wako.
“Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja”
 (Mwanzo 2:24)
Watu wengi nimeona hasa wasichana wanapokuwa wametoka kuolewa tu! anaanza kupungua mwili, na siyo kwamba hali chakula, bali anakuwa na mawazo na kutokusahau nyumbani, kama hauna msuli wa kusahau wazazi nakwambia usiwe na halaka ya kuolewa subiri kwanza uondoke umekomaa, na hii huwa inaathiri sana wanadoa kwani mwanamume hawezi kumtamani mke wake vile inavyotakiwa, yaani ataonekana kama anamlazimisha hasa pindi wanapoingia faragha ya ndoa, inafika hata wakati wa kula chakula huwa inakuwa ni ngumu kidogo kwa mtu ambaye bado hajasahau nyumbani.
        Unapokuwa unaambatana na mkeo/mumeo inamaana mnakuwa na nia moja, dhumuni moja ili kufikia malengo katika ndoa yenu na pindi matatizo yanapotokea ni rahisi kuyamaliza nyie wenyewe, kunatatizo moja ambalo linasumbua sana ndoa changa, ni pindi tu wanapokorofishana tena sababu yenyewe ni ndogo sana ambayo mnaweza kuitatua nyie wenyewe kwa kukaa chini, utashangaa mwanamke anatoa taarifa nyumbani mara moja, na siku hizi kuna Simu, hivyo atapiga Simu kwa ndugu zake wote na kama wanaishi karibu na nyumbani uwe na uhakika ataenda nyumbani ama ndugu zake watakuja ilimradi wapate taarifa vizuri, lakini madhara yake ni makubwa sana kwani utakuja kujutia mwenyewe hapo baadaye. Ujue watatokea washauri ambao watakushauri vibaya juu ya ndoa yako, pili watatambua madhaifu yenu katika ndoa kitu amabacho siyo vizuri.
         Nilikuwa mkoa fulani sitaki kuutaja, nikawa kwenye huduma na mara nikaitwa na dada mmoja aliyekuwa ni mtumishi mwenzangu ili nimsikilize yule kaka aliyekuwa amekaa naye, na shida yake yule kaka, nilipomsikiliza alisema hivi, alikuwa na mke na huyo mke alimkimbia kwa sababu ya ugonjwa wa mwanamume na huo ugonjwa ni kwamba alikuwa anakojoa kitandani na alisema ukweli yule kaka, lakini nilipoendelea kuhojiana naye nikatambua kwamba yule mke alishawishiwa na wazazi wake, na kwa sababu aliwashirikisha wazazi wake jambo la mume wake ndiyo mana wakamshauri amwache. Lakini Mungu ni mwema yule kaka tukamwombea na akafunguliwa na ile hali ya kukojoa ikaisha na baada ya muda akapiga simu kwamba amepata mchumba mwingine.
         Unapoambatana na mkeo na kuwaacha wazazi wako mnatakiwa kushirikishana nyie wenyewe kwa kila kitu, usije kumficha jambo mwenzi wako. Kuna ndoa fulani ni mpya tu na niwapendwa katika Kristo lakini mwanamume hataki kabisa kumshirikisha mke wake, hata juu ya mshahara anaoupata hataki kumwambia mke wake, ila kanisani anaweza akapeleka sadaka hadi Laki tano, na yeye kwake ni kawaida na huwa wanaingia mpaka kwenye ugomvi na mke wake kwa kupigana kabisa tena wanapelekana mpaka hospitalini, sasa unategemea kunabaraka zitakuja kweli hapo, angalia Petro anavyosema;
Kadhalika ninyi waume kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu, na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusikilizwe” (1Petro 3:7)
Uwe na uhakika ndoa isipokuwa na amani, baraka zinazoingia hapo zinakuwa ni butu, sasa kama moyo wako utaendelea kuambatana na wazazi ukiwa bado uko ndani ya ndoa yako ujue hamtaweza kuelewana na mke/mume wako kwa sababu hamtakuwa na nia moja, kila mtakaloshauriana hamtaafikiana kwa sababu ukifikilia hilo jambo likitendeka utahamishwa pengine kikazi na itakupelekea kwenda mbali na wazazi. Nakumbuka kaka mmoja alinifuata akaniambia shida yake halafu nikamuuliza mke wako yuko wapi? Akaniambia alikataa kuhama pamoja na mimi kwa sababu mama yake huwa anamsaidia kazi ndogondogo pale kijijini. Sasa inamaana huyu mwanamke hajatimiza neno “kuambatana”.
          Suala la mzazi anapokuja kuwatembelea nyumbani na kumbadilisha kuwa ni mwanamke wa kazi hiyo siyo tabia nzuri, kunandoa moja haikuwa na mahusiano mazuri kati ya mke na mume, ikafika mama wa mwanamume akawa yupo pale nyumbani kwa kitambo kidogo, cha ajabu nikwamba yule baba alikuwa anampatia mama yake mzazi pesa za mahitaji ya pale nyumabani kama ni sokoni na kila kitu, yaani yule mama ndiye aliyekuwa ni mpangaji wa kwamba leo mtakula hiki au hiki, sasa mke mwenye nyumba hakuwa na sauti jambo ambalo likapelekea mpaka kutengana mpaka sasa. Jihadhari sana kijana uliye kwenye ndoa na wewe unaetaka kuingia kwenye ndoa.


Itaendelea...............

+255 (0) 712 201 073/ +255 (0) 752 005 418