MAJIBU YA MUNGU KWA MAOMBI YAKO

       Maombi yanaweza kupata “Ndiyo” kama umeomba sawa sawa na mapenzi ya Mungu, na maombi mengine yanaweza kupata jibu la “Hapana”, kama hatuyaombi sawasawa na mapenzi yake, au kama Mungu haoni uzuri wa kutujibu sala zetu kama tulivyoomba, “Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia” (1Yoh 5:14).  Biblia inasema: “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tama zenu” (Yak 4:3). Kila mmoja wetu, anatakiwa kuomba vizuri ili Mungu ampe jibu la ndiyo na wala si la hapana kwa maombi yake yote. Kuna umuhimu wa kumtafuta sana Mungu na kumjua ili upate kufahamu yaliyo mapenzi yake kwako kusudi uombe sawa sawa na mapenzi yake, “Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyomapenzi ya Bwana” (Efe 5:17).
         Mungu anaweza kumpa mtu jibu la hapana kutokana na hekima yake mwenyewe. Paulo aliomba apone mwiba, au udhaifu wa afya aliokuwa nao na Mungu akamwambia: “Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu” (2Kor 12:9). Hivyo, Paulo aliendelea kuwa na mwiba huo ila Mungu alimsaidia kustahimili. Siyo kila uhitaji au masumbufu yanayokukumba ukadhania Mungu hayaoni, Hapana! Anayaona na anasikia unapokuwa unaomba, lakini anahitaji uendelee kukaa mbele zake kwani anamakusudi maalumu na wewe, mpaka wakati utakapofika wa kile alichokukusudia, atakuonesha na kukupatia.
      Maombi mengine, yanaweza kupata jibu la “Subiri”, maana, Mungu kwa hekima yake, anaweza kuona ni vyema mtu asubiri kwanza, kuliko kumpa jibu la ndiyo wakati huo. Naamini Ibrahimu na Sara walikuwa wakimwomba Mungu awape mtoto lakini, Mungu aliwapa katika kipindi alichotaka yeye, Ibrahimu akiwa na umri wa miaka 100 na Sara miaka 90 (Mwa 21:5), japo ahadi ya kumfanya Ibrahimu kuwa taifa kubwa, kwa kupitia uzao wake ilitolewa wakati Ibrahimu akiwa na umri wa miaka 75 (Mwa 12:1-4). Mfano mwingine ni huu: kijana mdogo anaweza akamwomba Mungu ampatie mke au mme. Mungu atamwambia subiri kwanza. Hivyo, tukiona kuwa Mungu hatupi yale tuliyoomba, tusidhani kuwa Mungu amesema “Hapana” huenda anatutaka tusubiri kwanza.
       Mungu pia, anaweza akatupa jibu la “Fanya hivi kwanza, ndipo upate ulichoomba”. Mfano, yule kipofu aliyeomba aponywe upofu wake, alipakwa tope machoni, na kuambiwa aende akanawe kwenye bwawa la Siloamu, ndipo apate kuona (Yoh 9:6-7). Vipofu wengine waliguswa tu na Yesu, wakaona, na wengine wala hawakuguswa, ila waliambiwa na Yesu, “Imani yako imekuponya:, nao wakaona, ila huyu alipewa jambo la kufanya kwanza ndipo apate kuona. Alikwenda kwenye bwawa la Siloamu, lile aliloambiwa na Yesu, aliponawa, akaanza kuona.
        Naamani aliambiwa akaoge mara saba ndani ya maji ya mto Yordani, ndipo apone ukoma wake (2Fal 5:10). Naamani hakukubaliana na majibu ya maombi yake, kwa mara ya kwanza, lakini baada ya kupewa ushauri na kulitimiza lile sharti, la kuoga mara saba akatakasika. Hivyo, Mungu akituagiza kufanya kitu Fulani kwanza, tukifanye, naye atatufanyia tuyaombayo.
         Mungu pia, anaweza akakujibu maombi yako kwa kukupa kile unachokiomba, kwa kutegemeana na msimamo wako binafsi, hata kama siyo mpango wake. Mara nyingi Mungu hapendi kuingilia maamuzi na misimamo ya mwanadamu, hivyo anaweza akakupa kitu unachokiomba lakini kikakuharibia maisha yako, Bali walitamani jangwani, wakamjaribu Mungu nyikani. Akawapa walichomtaka, akawakondesha roho zao” (Zab 106:14-15). Mungu huwa anapenda sana kuonekana kwa mtu amtafutaye kwa bidii, hasa mtu anapoomba jambo Fulani, Mungu anapenda ajitukuze kwa kumjibu yule mtu, ili kiwango cha imani ya yule mtu kipande, lakini wengi tunaomba vitu ambavyo siyo wakati wake, wala mazingira yako kuweza kubeba hicho kitu hauna. Wengi wamefanikiwa, wakaacha hata kwenda kanisani, wengine wakipata mafanikio wanaanza kunyanyasa wake zao, waume zao, majirani zao, mpaka ndugu zake. Kwa sababu uko hivyo, basi roho yako itakonda na hutauona ufalme wa Mungu.

         Yapo mambo ya muhimu kuyataja kwenye sala zetu. Unaposali, usitoe shida zako tu bila ya kusema mambo mengine kwanza. Anza sala yako ya kumtukuza Mungu. Sala ya BWANA ni kielelezo chetu. Sala hiyo inaanza kwa maneno haya: “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje” (Mt 6:9). Ni muhimu sana kuanza na kumtukuza Mungu, maana, anastahili kutukuzwa, na kuhimidiwa, mana bila yeye, hakuna kitu chochote kilichopo ambacho kingeliweza kuwepo. Yeye ameumba vitu vyote, na anaendeleza kuwepo kwa vitu vyote.
      Baada ya kumtukuza Mungu, tunatakiwa kuungama dhambi zetu. Kama tutamwomba Mungu, bila ya kuungama dhambi zetu, Mungu hatasikia, maana dhambi, inaleta utengano kati ya mtu na Mungu. Yatupasa tuungame, tuwe safi kiroho, ili Mungu wetu, atusikilize sala zetu. Neno la Mungu linaongea juu ya Mungu kutokujibu sala zetu kwa sababu ya dhambi zetu kwa kusema: “Tazama, mkono wa BWANA haukupunguka, hata usiweze kuokoa; wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia” (Isa 59:1-2).
         Mara nyingi, sisi wanadamu, huanguka dhambini na dhambi zetu, ndizo zinazotutenga na Mungu wetu. Yatupasa kukiungama kile kinachotutenga na Mungu kwanza, ili uhusiano wetu na Mungu urudi, ndipo tumwombe Mungu atusaidie kama yalivyo mapenzi yake.
          Kitu cha tatu kwenye sala, ni kumshukuru Mungu, kwa mema yote aliyotutendea. Daudi alikuwa akimshukuru Mungu kwenye sala zake. Daudi alitunga wimbo unaosema: “Mshukuruni BWANA kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele” (Zab 136:1). Sehemu nyingine, Daudi alimshukuru Mungu kwa kusema: “Nitakushukuru kwa moyo wangu wote” (Zab 138:1). Mungu ametutendea  mambo mengi sana. Kama hatutamshukuru katika sala zetu, tutakuwa watu wasio na shukurani, wasiouhesabu wema wa Mungu kuwa ni kitu chema kwao. Wapo watu wengi sana, wanaougua, na hata kufa, wengine wanakosa chakula au mahitaji mengine, na wengi wana shida za kila aina, ila wengine, wanaishi salama. Na ikumbukwe kuwa, hatuishi salama kwa sababu ya wema wetu, bali fadhili za Mungu, ni nyingi sana kwetu, hivyo, tunahitajika kumshukuru sana Mungu.
         Daudi alipoangalia ulinzi wa Mungu kwake, wema wake wote aliomtendea, alisema: “Nimrudishie BWANA nini, kwa ukarimu wake wote alionitendea?” (Zab 116:12). Yatupasa kumshukuru sana Mungu kwa wema wake wote aliotutendea. Kama hatutamshukuru, tutakuwa kama watu wa siku za mwisho, “wasio na shukurani” (2Tim 3:2). Watu wanaoona ni haki yao kufanyiwa, wanayofanyiwa na Mungu, wakati kufanyiwa tunayofanyiwa ni upendeleo, kwa maana, wazazi wetu walioingia dhambini, waliingia kwa hiari yao wenyewe. Biblia inasema: “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zetu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye asije akajisifu” (Efe 2:8). Tunatakiwa kumshukuru sana Mungu kwa yote anayotufanyia, na wala tusijifanye kama hatuyaoni yale anayotufanyia.

         Kitu cha mwisho cha kutaja kwenye sala zetu, ni kutoa haja zetu kwa Mungu, ikiwemo na kuwaombea watu mbalimbali pamoja na wahudumu wa Injili, na wahitajii. Kila mmoja wetu anatakiwa kupeleka shida zake zote kwa Mungu, maana yeye anaweza kututatulia shida zote, maana Biblia inasema: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa” (Yoh 7:7-8). Lazima tutambue kuwa, hatuwezi kujiokoa sisi wenyewe, wala kujitatulia matatizo yetu sisi wenyewe (rejea Yoh 15:5). Yatupasa tumwombe Mungu atusaidie. Ukosefu wa imani kwa Mungu, ndio unaowafanya watu wengi wasimpelekee shida zao. Tuwe na imani naye, ili tumpelekee shida zetu, naye atatusaidia, sawa sawa na mapenzi yake.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni